Kurasa Muhimu

Friday, April 4, 2014


  TAARIFA YA KONGAMANO LA TISA LA CHAWAKAMA LILILOFANYIKA MJINI TANGA
MNAMO TAREHE 26/02/2014 HADI TAREHE 1/3/2014.
1.0 Utangulizi.
Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili Afrika Mashariki (CHAWAKAMA) kilianzishwa mwaka 2004 ambapo pamoja na malengo mengine, lengo kuu ni kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili Afrika na Duniani kwa ujumla. Ikiwa kama sehemu ya lengo la chama; makongamano mbalimbali huandaliwa kwa utaratibu maalumu ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuwaweka pamoja wanachama na wadau wengine wa lugha ya Kiswahili ili kuwatia chachu ya kuendeleza lugha hii adhimu na haushi.

Utaratibu wa uandaaji wa makongamano upo katika mawanda ya kimataifa (jumuiya) na kitaifa (kikanda) ambapo katika mawanda ya kijumuiya huhusisha nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki hivyo kwa kufuata muundo wa uandaaji, Kongamano la mwaka huu limepangwa kufanyika nchini Kenya. Kwa upande wa ndani ya nchi, makongamano haya hufanyika ndani ya nchi husika ambapo kongamano la mwaka huu liliandaliwa na kufanyika katika chuo kikuu cha Eckenforde mjini Tanga
1.1 Kongamano lenyewe.
1.1.1 Washiriki
Katika kongamano hili jumla ya washiriki wanachama 280 walihudhuria wakiwemo wahadhiri na wadau wengine wa lugha ya Kiswahili kutoka katika Vyombo vya habari, waalimu wa shule za sekondari na viongozi wa kiserikali. Pia baadhi ya mabwiji wa lugha hii walishiriki wakiwemo Prof. Msanjila, Mwansoko(aliyekua mgeni rasmi), Kiango, na Prof Senkoro

1.1.2 Uwasilishaji Mada
Mada zote zilizopendekezwa ziliwasilishwa. Mada hizo ni Mchango na changamoto za vyombo vya habari, Bunge na Wanataaluma katika kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili hapa nchini. Nini suluhisho la changamoto hizo?, lugha ya Kiswahili ni bidhaa adimu, jadili ni jinsi gani kijana atakavyoitumia kuleta maendeleo endelevu., Sharban Robert kama baba wa fasihi ya Kiswahili anayo nafasi gani katika fasihi ya zama hizi? na mchangamano baina ya asili ya Kiswahili na Mswahili.

1.1.3 Kauli Mbiu
Kauli mbiu ya mwaka huu ilikua ni MIAKA 52 YAUHURU, KISWAHILI TUNU YA KIJANA KWA MAENDELEO ENDELEVU. Kauli mbiu hii inamtia kijana hamasa ya kutumia lugha ya Kiswahili vyema katika kujiletea maendeleo yanayodumu.

1.1.4 Siku ya kwanza.
Siku hii ilianza kwa namna yake ambapo washiriki wote wakiongozwa na kikundi cha tarumbeta waliingia ukumbini kwa maandamano ya matembezi mafupi kiasi cha robo kilometa chini ya ulinzi wa jeshi la polisi. Baada ya kuwasili ukumbini washiriki pamoja na wageni walichukua nafasi zao ambapo utambulisho ulifanyika kasha risala ikasomwa na mwenyekiti wa CHAWAKAMA kanda Erasto Chan’ga na kufuatiwa na hotuba kutoka kwa mgeni rasmi Profesa Mwansoko.  Baadaye  tulipata ‘CHAASU’ kisha ikasomwa mada ya kwanza kutoka chuo wenyeji na  kuchangiwa na washiriki mbalimbali. Baada ya hapo tulipata CHAMCHA kisha mada moja binafsi ikasomwa na kuchangiwa na baadhi ya  wadau waliokuwepo. Baada ya wasilisho la mada hiyo ilifuatiwa na vitushi mbalimbali kutoka kwa wanachama hatimaye muda wa chajio nakufuatiwa na wasaa binafsi.


1.1.5 Siku ya pili.
Tulikutana ukumbini saa mbili kama ilivyo ada, kisha mada ya Mchangamano baina ya asili ya Kiswahili na Mswahili iliwasilishwa na wanachama kutoka chuo kikuu cha Zanziba SUZA na kuchangiwa na wadau mbalimbali. Baada ya hapo ilifuatia mada ya Shaban Robert kama baba wa fasihi ya Kiswahili na nafasi yake katika zama za hivi leo. Wasilisho liliandaliwa na kuwasilishwa na wanachama kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam ambayo iiwasilishwa makusudi kwa lengo la kujua wasifa wa nguli huyu kabla ya kwenda kuzuru makazi yake. Baada ya kupata  ‘chai nzito’ tulienda kuzuru nyumbani kwake (Machui) alipoishi na kuzikwa nguli wa fasihi Shabani Robert. Baada ya kufika kwenye makazi yake tuliwakuta wenyeji akiwemo mama mdogo wa marehemu  pamoja na mjukuu wake aliyetusimulia habari zake. Pamoja na kuzuru alipozaliwa, pia tulizuru mahali alipoishi, maktaba na alipopumzikia na kuuza machapisho yake maeneo ya ufukwe wa bahari ya hindi. Waaida Chama kwa kupitia harambee ndogo iliyofanyika, kilitoa zawadi ya vyakula vyenye thamani ya shilingi laki moja na sitini elfu (160000) kwa ndugu zake marehemu. Baada ya kurudi ukumbini tulipata burudani kisha Chajio na hatimaye uhuru binafsi.


1.1.6 Siku ya tatu.
Mada ya nne iliyokua inahusu mchango na changamoto za vyombo vya habari, Bunge, na Wanataaluma katika kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili hapa nchini iliwasilishwa kisha kuchangiwa na washiriki mbalimbali akiwemo mwandaaji wa vipindi vya Kiswahili TBC1 Victor Eliah ambaye pamoja na michango mingine alitoa wito kwa wanachawakama kushiriki katika kutangaza lugha ya Kiswahili kupitia runinga kwani nafasi zipo. Ilifuata chai nzito kabla ya safari ya kuzuru kwenye mapango ya kihistoria ya Amboni ambapo tuliona na kujifunza mengi kuhusu utamaduni wetu. Tuliporudi ukumbini tulipata wasaa wajiliwaza kwa burudani ambapo fursa ya kucheza na kughani mashairi ilitolewa, muda wa Chajio ulipowadia washiriki walijipatia na wasaa wakujinafasi ulifuata.

1.1.7 Siku ya nne.
Kama ilivyodesturi kwa wakazi wa mji wa Tanga wa kufanya kazi ya usafi kwa pamoja kwa kila jumamosi ya kila mwisho wa mwezi, nasi hatukubaki nyuma kwani kitu kizuri kula na mwenzako, wanatanga walitualika ambapo pamoja na wakazi wengine mkuu wa wilaya ya Tanga Mjini alitupa shavu. tulishiriki usafi katika eneo la kiwanja cha mpira wa miguu cha Mkwakwani pamoja na maeneo yaliokizunguka.
Baada ya usafi, wanachama walienda ufukweni kuzuru eneo ambalo Shaban Robert alikua anauzia machapisho yake, wakapata ‘chai nzito’ huko ambapo viongozi wote wa matawi, kanda na wa Afrika Mashariki walikua na kikao eneo jirani na hilo. Kama wanenavyo wahenga hakuna marefu yasiyokua na ncha, ilpotumi saa sita mchana tulirudi ukumbini na ilipojiri saa saba mchana  Profesa Mwansoko alitamatisha kongamano la tisa la CHAWAKAMA kitaifa kwa  nasaa yake fupi iliyotamalaki hekima za kitaaluma.
2.1 Mafanikio.
Kutokana na yaliyojiri katika kongamano, kama ilivyoripotiwa hapo juu ni wazi kwamba limeacha alama za ushindi na funzo kwa wangenzi walioshiriki.
2.1.1 kongamano hili limetoa nafasi ya kipekee kwa wadau washiriki kumjadili kwa kina aliyekuwa mwandishi wa kazi za kifasihi hayati Shaban Robert kwa njia ya makala na uwandani.
2.1.2 Kongamano hili limefanikiwa kuwa kongamano la kihistoria kwani wanachama waamefanikiwa kutembelea maeneo mbalimbali ya kihistoria kama vile kwenye Mapango ya Amboni.
2.1.3 Pia kongamano limeamsha ari kwa wadau mbalimbali wa Kiswahili katika kuendeleza na kukuza lugha ya Kiswahili popote Duniani kwani lilifanikiwa kuwaweka pamoja wadau wote wa lugha ya Kiswahili na kuwatia hamasa ya kueneza lugha hii ya Kiswahili.
2.1.4 Uwasilishwaji wa mada umejenga changamoto kwa wanagenzi wa lugha hii adimu kubuni na kurekebisha makosa katika kukiendeleza Kiswahili. Kwa mfano mada ya changamoto za wa Bunge, Wanataaluma na Vyombo vya habari linatoa nafasi kwetu kama wanataaluma kuboresha lugha yetu katika Nyanja tajwa.
3.1 Changamoto.
Kama wanenavyo wahenga ‘Hakuna kapa isiyokuwa na usubi’ Pamoja na kuwepo kwa mafanikio makubwa katika kongamano hilo, pia kulikua na baadhi ya changamoto.
3.1.1 Changamoto hizo ni pamoja na kutokuwepo kwa sehemu nzuri za malazi. Mazingira ya  kulala yalikua ni shida kwani baadhi ya watu hawakuzoea kulala kwenye mazingira kama yale na hivyo kusababisha kwenda kulala kwenye vyumba vya wageni kwa gharama zao.
3.1.2 kutokujitosheleza kwa ratiba ambapo baadhi ya matukio yaliyooneshwa kufanyika, hayakufanyika. Kwa mfano, ratiba ilikua inaonesha kungekuwepo na burudani kutoka kwa wasanii kama akina Mrisho Mpoto pamoja na Mzee Majuto lakini hatukufanikiwa kuwaona wala kupata burudani kutoka kwao.
4.1  Mapendekezo.
Mambo yafuatayo yanapendekezwa ili kuboresha makongamano yajayo;
4.1.1        Suala la malazi liandaliwe na kudhibitisha ubora kabla ya siku ya kongamano.
4.1.2        Matukio yatakayokua yameandikwa kwenye ratiba yawe yamethibitishwa kwamba yatakuwepo.


                         IMEANDALIWA NA ABEL PATRICK- KATIBU CHAWAKAMA CKDSM

                     IMEHARIRIWA NA ATHANAS BARNABA- MHARIR CHAWAKAMA CKDSM

1 comment:

  1. Napenda kuwapongeza CHAWAKAMA CKDSM kwa juhudi zenu mnazozifanya za kueneza lugha ya Kiswahili kwa njia ya makongamano, nimatumaini yangu kuwa mtakuwa wenyeji wa kongamano lijalo. Ahsanteni.

    ReplyDelete